Friday, 8 February 2008

MIZENGO PINDA ATEULIWA WAZIRI MKUU

Rais Jakaya Kikwete amemteua Mhe. Mizengo Kayanza Peter Pinda Mbunge wa Mpanda Mashariki (CCM) kuwa Waziri Mkuu mpya kuchukua nafasi iliyoachwa wazi kufuatia kujiuzulu kwa aliyekuwa Waziri Mkuu Bw. Edward Lowassa aliyejiuzulu jana baada ya kuhusishwa na kashfa ya Richmond.
Jina la Mhe. Pinda lilitangazwa Bungeni na Spika wa Jamhuri ya Muungano Mhe. Samuel Sitta mara baadaya kufungua bahasha iliyokuwa na jina hilo. Mara baada ya spika kutaja jina la Waziri Mkuu huyo mteule ukumbi wa Bunge umelipuka kwa kushangilia.
Mhe. Pinda alizaliwa mwaka 1948 huko Mpanda na baada ya elimu ya awali aliendelea na kupata shahada ya sheria toka Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam. Baadhi ya nyadhifa alizowahi kushika ni pamoja na kuwa Ofisa Usalama wa Taifa, Mwanasheria wa Serikali, Katibu Msaidizi wa Rais na Katibu wa Baraza la Mawaziri.
Kabla ya wadhifa wake huo Mpya, Bw. Pinda alikuwa ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI). Uchaguzi wa Mhe. Pinda unaonesha kuwa Rais Kikwete ameamua kwenda na chaguo salama zaidi hasa kwa vile Mhe. Pinda alikuwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu aliyejiuzulu kufuatia kashfa ya Richmond.
Bado haijajulikana mwitikio wa wananchi na wachambuzi ya mambo ya kisiasa kuhusu uteuzi huo wa Bw. Pinda. Hata hivyo inatarajiwa kuwa Mhe. Pinda ataweza kufanya kile ambacho Mhe. Lowassa alishindwa.
KLH News inamtakia kila la kheri Mhe. Pinda katika wajibu wake huo mkubwa katika kuitumikia nchi yetu.

Thursday, 7 February 2008

LOWASSA AJIUZULU

Waziri Mkuu Lowassa ajiuzulu juu ya kashfa

"Nimeamua kumwandikia Rais barua ya kumwomba niachie ngazi."
Sikiliza Leo Afrika
Waziri Mkuu wa Tanzania Edward Lowassa amejiuzulu baada ya kulaumiwa na kamati ya bunge iliyochunguza kashfa ya ufisadi mkubwa katika utolewaji zabuni ya umeme wa dharura.
Akitangaza hatua yake katika bunge Alhamis asubuhi, Bwana Lowassa alisema: "Nimetafakari sana kwa niaba ya chama changu, kwa niaba ya serikali yangu, nimeamua kumwandikia Rais barua ya kumuomba niachie ngazi."
Hatua ya kujiuzulu
ninafanya hivyo kwa moyo mweupe kabisa

Waziri Mkuu Lowassa
Bwana Lowassa aliteta kwamba kamati teule ya bunge iliyomhusisha na kashfa ya Richmond ilimnyima haki ya kujieleza.
Alisema alikuwa ametafakari kwa makini kuhusu shutuma hizo na kufikia uamuzi kwamba, "tatizo ni uaziri mkuu."
"Kwamba ionenekane Waziri Mkuu ndiye amefanya haya, tumwondolee heshima au tumwajibishe."
Akielezea hatua yake ya kujiuzulu, Bwana Lowassa aliongeza "ninafanya hivyo kwa moyo mweupe kabisa ili kuonyesha dhana ya uajibikaji na pia kutokukubaliana na utaratibu uliotumika kusema uongo ndani ya bunge kwa kumsingizia mtu."
Nguvu kubwa
Zabuni hiyo ilipewa kampuni ya Richmond Development group yenye makao yake nchini Marekani.
Kamati teule ya bunge kwenye ripoti yake iliyowasilishwa hapo Jumatano, ilipendekeza kujiuzulu au kuchukuliwa hatua kali kwa wahusika.
Ripoti hiyo iliwasilishwa bunge na Mwenyekiti wa kamati hiyo teule, Harrison Mwakyembe.
Kuhusu Waziri Mkuu, ripoti hiyo inasema: "Uamuzi wa serikali kuizuia Tanesco ( Shirika la umeme Tanzania) isivunje mkataba na kampuni hiyo licha ya sababu zote za kisheria kuwepo ni baadhi tu ya viashiria vya nguvu kubwa iliyojuu ya wizara ya nishati na madini."
Waziri Mkuu akosolewa
Kutokana na ushahidi wa kimaandishi, kimazingira na wa kimdomo inaiona nguvu hiyo kuwa ni Waziri Mkuu

Kamati teule ya bunge
"Kutokana na ushahidi wa kimaandishi, kimazingira na wa kimdomo inaiona nguvu hiyo kuwa ni Waziri Mkuu."
Kikatiba ndiye mwenye madaraka ya juu ya udhibiti, usimamiaji na utekelezaji wa siku hadi siku wa kazi na shughuli za serikali.
Yeye pia ndiye kiongozi wa shughuli za serikali bungeni.
"Kamati teule haikufurahishwa hata kidogo na taarifa hizo zinazomgusa moja kwa moja Mheshimiwa Waziri Mkuu katika kuipendelea Richmond."
Ubadhirifu na rushwa
Mawaziri wengine walioshutumiwa katika ripoti hiyo ni yule anayehusika na nishati na madini, Nazir Karamagi, mtangulizi wake Dr. Ibrahim Msabaha ambaye sasa ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa takukuru, ilikuwa motoni kwa kutoa maelezo ya uongo kwa kamati hiyo.
Serikali ya Rais Kikwete imeahidi kupambana na rushwa
Mbunge Mwakyembe alisema kamati yake ilitaka kuweka wazi kwamba mchakato wa zabuni ya kuzalisha nguvu za umeme kwa dharura wa megawati 100 ulighubikwa na vitendo vya ukiukwaji taratibu, kanuni na sheria za nchi."
"Na hivyo kujenga kiwingu cha mashaka ya upendeleo, ubadhirifu na rushwa ambavyo vimechangia kumwongezea mwananchi mzigo wa gharama za umeme."
Takukuru yashutumiwa
Taifa lilikuwa limetumbukizwa kwenye hasara kubwa kutokana na mkataba huo wa Richmond kinyume na taarifa iliyotolewa na Takukuru (taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa).
Uongo wa Richmond
Kwa nini kamati ya wataalamu haikuihoji Richmond kuhusu uongo huo bayana?

Kamati teule ya bunge
Ilishutumiwa kwa kujiharibia sifa yenyewe baada ya kutoa ushahidi wa uongo ikisema mchakato wa zabuni hiyo ulikuwa wazi, shirikishi na ulizingatia kanuni na kwamba dosari zilizojitokeza hazikuhitimu kuiletea taifa hasara.
"Taarifa hiyo imemong'onyoa kwa kiasi kikubwa hadhi na heshima ya chombo hiki muhimu cha kitaifa kilichopewa dhamana ya kupambana na rushwa na siyo kuipamba ili kurejesha heshima ya umma katika taasisi hiyo."
Richmond ilidai kuwa na miradi mikubwa Tanzania
Kamati hiyo ilipendekeza mabadiliko ya haraka ya uongozi wa taasisi hiyo.
Mbunge Harrison alisema kwenye tovuti yake, kampuni ya Richmond "ilikuwa inajitangaza kimataifa kipindi hicho kuwa kampuni yenye miradi mikubwa Tanzania ya ujenzi wa kiwanja cha kisasa cha michezo, ujenzi wa bomba la mafuta la kilomita 1150 na ukarabati wa viwanja kadhaa vya ndege nchini."
Kamati teule ilishindwa kuelewa "kwa nini kamati ya wataalamu haikuihoji Richmond kuhusu uongo huo bayana ambao uliokuwa ushahidi wa kutosha kuipotezea sifa za kuwa mzabuni?"

Monday, 4 February 2008

WATANZANIA WANAPASWA KUMPOKEA RAIS BUSH KWA MABANGO


Watanzania wanapaswa kumpokea Rais Bush kwa mabango
Raphael Mgaya
HAKUNA shaka ukweli ni nguvu! Ni silaha dhidi ya uongo. Katika kila jamii, tangu kale, tabaka tawala huhodhi vyombo vya habari na njia zozote za kusambaza taarifa ili kulinda mfumo uliopo.
Mfumo wa kihafidhina, kandamizi na nyonyaji hutumia vyombo vya habari kueneza uongo na propaganda ili kudanganya umma na kudumaza harakati za kupambana na tabaka tawala.
Hadi tu umma utakapopata fursa ya kupata mawazo na taarifa sahihi, ndipo utakapogeuka na kuwa nguvu itakayoweza kuleta mapinduzi yatakayoung'oa mfumo uliopitwa na wakati na kandamizi uliopo madarakani!
Nimesoma taarifa kuhusu ujio wa Rais wa Marekani nchini Tanzania na nchi nyingine za Afrika. Nimesoma pia taarifa ya John Chiligati, Katibu wa Itikadi ya Uenezi wa CCM, ikidai kuwa "ziara hii tuitumie kuimarisha uhusiano wetu na Marekani, wananchi wajiandae katika ugeni huu mkubwa".
Chiligati ametoa pia takwimu ya misaada ya kifedha ambayo Marekani imeisaidia Tanzania, ambao ukiziangalia kwa juu juu, bila kuzingatia masuala mengine muhimu, Watanzania wengi bila shaka watadhani Marekani au Rais Bush ni msamaria mwema!
Taarifa ya CCM, inaonyesha namna ambavyo tabaka la mabwanyeye ndani ya nchi (national bourgeois class) linavyoshirikiana na mabwanyeye wa kimataifa (international bourgeoisie) katika kuendeleza unyonjaji wa umma na mali za nchi zilizonyuma kiuchumi kwa masilahi ya ubepari.
Lengo la taarifa ya CCM ni kuwapotosha Watanzania kutoka kwenye masuala nyeti yanayohusu ukombozi wao na badala yake wajishughulishe na namna ambayo watamfurahisha Bush ili awaongezee misaada!
Katika nchi nyingi anakotembelea Rais Bush, anakutana na upinzani mkali sana kutoka kwa wanachi, si watawala. Mwaka jana Bush alipotembelea Marekani ya Kusini, alikutana na upinzani wa kihistoria kutoka kwa wananchi wa Venezuela, Argentina, Brazil, n.k.
Wanachi wa Marekani ya Kusini walitumia fursa zao kumwabia Bush ukweli. Walimpokea kwa mabango wakisema 'komesha ubeberu wa Marekani', 'Komesha vita vya mafuta', 'funga jela ya Guantanamo' n.k.
Wakati Bush akipambana na upinzani mkali, Hugo Chavez, mwanamapinduzi, Rais wa Venezuela, alipokewa kwa shangwe za vigelegele na milio ya risasi na mamilioni wanachi kokote alikokwenda Amerika ya Kusini kama ishara ya kumuunga mkono katika harakati zake za kukomesha ubepari na ubeberu wa Marekani duniani.
Hakuna nchi inayoweza kuendelea kwa misaada duniani. Hata historia imeonyesha kuwa nchi zote zilizoendelea, zimeendelea kwa kutumia rasilimali zilizopo ndani ya nchi, ardhi, madini, maji, misitu n.k. kwa kutumia teknolojia, ujuzi na elimu iliyopo.
Hata Mwalimu Nyerere alituasa kuwa jamii haiwezi kuendelezwa, bali inaweza kujiendeleza yenyewe! Misaada ambayo Marekani inaipa Tanzania haina maana kabisa ikilinganishwa na taabu, adha na mateso ambayo Watanzania na watu wengi duniani wayapata kwa sababu ya dhuluma za ubeberu wa Marekani na washirika wake!
Kwa bahati mbaya, tofauti na sehemu nyingi duniani, Afrika tuko nyuma katika utashi wa kisiasa na hali halisi ya mambo duniani kutokana kwanza na watawala wetu na pili kutokana na historia yetu.
Ndiyo maana, wengi hawajui dhuluma ya Marekani duniani. Na kwa mantiki hiyo, taarifa ya CCM, inaweza ikawafanya Watanzania wengi kumpokea Bush kama mkombozi, na si vinginevyo! Ni kwa sababu hiyo hiyo, nina wasiwasi kuwa upinzani alioupata Bush sehemu nyingi duniani anaweza asiupate Afrika.
Mataifa mengi yanashindwa kuendelea kwa sababu ya mfumo wa kinyonyaji uliopo duniani. Marekani ndilo taifa linalohodhi mfumo huu na linatumia gharama kubwa kuhakikisha linaulinda.
Moja ya misingi ya mfumo huu ni biashara huria. Biashara huria ni moja ya sababu za kufukarishwa kwetu. Shirika la Biashara Duniani (World Trade Organisation-WTO) linaruhusu nchi tajiri kilinda masoko yake dhidi ya bidhaa rahisi kutoka nchi masikini ambazo nyingi ziko Afrika.
Kwa kufanya hivi nchi maskini hazipati masoko ya bidhaa zao za kilimo, nguo, n.k ambazo ndio msingi wa maendeleo. Kwa upande huo huo nchi maskini zinalazimishwa kufungua mipaka yako kuruhusu bidhaa kutoka nje, matokeo yake ni kuwa nchi masikini zimekuwa masoko ya nchi tajiri.
Hali kadhalika, nchi tajiri zinatoa ruzuku kwa wazalishaji wake na matokeo yake ni wazalishaji hawa kuzalisha bidhaa ambao zinauzwa bei ya chini katika soko la dunia huku bidhaa kutoka nchi masikini zikishindwa ushindani kwa kuwa bei yake ni kubwa kwa sababu ya gharama za uzalishaji.
Kwa maneno mengine hakuna haki katika biashara huria. Kwa mujibu wa taarifa ya UNCTAD - Tume ya Umoja wa Mataifa ya Biashara na Maendeleo - kama vikwazo hivi katika biashara vingeondolewa, nchi masikini zingeongeza kipato kwa dola la Marekani billioni 700 ambazo ni sawa na mara 13 ya misaada yote ya maendeleo duniani kwa mwaka!!
Kama unyonyaji huu ulioletwa na WTO ungekomeshwa, umasikini ungekuwa umepungua sana duniani, badala ya kuongezeka kama ilivyo leo.
Aidha, licha ya upinzani mkali duniani kote, Rais Bush aliivamia Iraq mwaka 2003 ili kudhibiti uzalishaji wa mafuta na Usambazji wa mafuta Iraq. Vita vya Iraq vimegharimu maisha ya watu takribani laki saba (700,000).
Hali ya Iraq si shwari, watu wengi wanaendelea kupoteza maisha, vita vimeacha yatima, wajane na walemavu kwa maelfu. Kudhilisha dunia ubabe wake, mshirika wake, Tony Blair (Waziri Mkuu mstaafu wa Uingereza, aliyemuunga mkono kuivamia Iraq) sasa ameteuliwa kuwa mshauri wa Benki ya J. P. Morgan, Benki ya Marekani ambayo imepewa jukumu la kuiendesha Benki Mpya ya Iraq!
Hapa inaonyesha jinsi tabaka tawala linavyoshirikiana na tabaka la kibepari katika kuendeleza masilahi ya ubepari na ubeberu wa Marekani.
Maovu ya Marekani ni mengi, si rahisi kuyaeleza yote katika ukurasa huu,. Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) ndiyo lililosababisha Nelson Mandela kutiwa mikononi mwa makaburu na hatimaye kuishi miaka 27 gerezani! Donald Richard aliyekuwa ofisa wa CIA Afrika ya Kusini, akijifanya ofisa balozi mjini Durban, akawataarifu polisi wa makaburu mahali ambako wengemkuta na kumkamata Mandela. Ikimbukwe pia kuwa, Bush (Mkubwa) alikuwa ndiye Afisa Mkuu wa CIA kipindi hicho!
Ni Marekani inayojitia kutoa misaada ya ukimwi ambayo iliongoza makakati wa mataifa ya Magharibi ya kuzuia ulegezaji wa masharti ya sheria ya hati miliki (Trade Related Intellectual Property Rights) ili kuziwezesha nchi masikini kuanzisha viwanda vya kutengeneza madawa ya kupunguza makali ya ukimwi.
Marekani kwa kushirikiana na Ubelgiji wanadaiwa kumuua Patrice Lumumba, Waziri Mkuu wa Kwanza wa Kongo sasa DRC na kumweka madarakani dikteta Mobutu Sseseko. Marekani ndio taifa lililo mstari wa mbele katika kuisaidia kwa moyo, kifedha na kwa kuipa silaha Israeli katika mpango wake wa kuwakandamiza Wapalestina.
Ni Marekani inayochafua mazingira kwa kiasi kikubwa duniani, taifa ambalo limekataa kuridhia itifaki ya Kyoto inayohusu kuzuia uchafuzi wa mazingira.
Licha ya maovu yote ya Marekani, bado watawala wetu wanazidi kujikomba kwa Marekani? Inakuwaje Kikwete mara baada ya kuchaguliwa kuwa rais, haraka haraka alikwenda kwa Bush, eti kujitambulisha? Inakuwaje baada ya kampeni baadhi ya wanasiasa wanakwenda kwa Bush na wanaporudi wanaeleza Bush amewasifu kuwa wamefanya kampeni vizuri?
Nalazimika kuamini kuwa watawala wetu wanamtazamo na uelewa finyu kuhusu hali halisi ya mambo duniani. Mwalimu Nyerere alikuwa mkali kwa kuwa alikuwa akijisoma sana, hivyo alipata kujua hali halisi ya mambo duniani. Watawala wetu leo nadhani hawasomi, kazi yao ni ziara za kuzunguka tu kama wanyapara.
Afrika ndilo bara pekee linalozidi kuwa masikini wakati mataifa mengine yanazidi kuendelea, tusipojihadhari tutaendelea kuwa nyuma milele.
Ni wakati wetu sasa wa kukasirika na kuamka na kusema sasa basi, tumechoka na watawala mamluki na manyapara. Na kwamba hatutaki kuendelea kunyonywa na mataifa ya kibepari. Inawezekana kuwa masikini na ukaheshimika.
Ningelikuwapo Tanzania wakati wa ujio wa Rais Bush ningeliandamana (hata peke yangu) kumpinga. Lakini, nadhani Watanzania wanapaswa kuniunga mkono, viongozi wa nyama vyote vya siasa pamoja ikiwamo CCM. Viongozi wa NGO hamasisheni wananchi wajitokeze kumpokea Bush kwa mabango ya kuwalilia yatima na wajane wa Iraq, kuwalilia wagonjwa na yatima wa ukimwi, kujililia wenyewe kwa sababu ya umasikini uliopandikizwa na Marekani na mataifa mengine ya kibepari na kupinga uchafuzi wa mazingira.
Watanzania, tumieni fursa hii kumweleza Bush kuwa misaada anayoipa Tanzania anarudisha sehemu ndogo tu ya kile anachotuibia sasa na kile ambacho mababa zetu wa kale waliochukuliwa kama watumwa walikizalisha!
Mwandishi wa makala hii ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Warwick, Uingereza.
Anapatikana kwa Barua pepe: b.t.mgaya@warwick.ac.uk

Sunday, 3 February 2008

NALAZIMIKA KUKASIRIKA NA KUKASIRISHWA KWA RAIS

Kizimba cha hoja:Nalazimika kukasirishwa na 'kukasirika kwa Rais.'



]
Na Hassan Abbas
NI wazi kuwa msomaji wangu makini hasa wale wanaofuatilia sana safu hii watashangaa kwa nini leo nakasirishwa na kukasirika kwa Rais? Mshangao huo utakuwa mkubwa zaidi kwa wale ambao walisoma makala yangu iliyokuwa na kichwa cha habari "Rais Kikwete:Haya ndiyo maslahi ya taifa." Katika makala hiyo nililidadavua sakata la mabilioni yaliyopotea Benki Kuu na kwenda mbali zaidi ya kumpongeza Rais kwa kuchukua uamuzi mzito, niligusia haja ya yeye kwenda mbali na kuhakikisha mabilioni hayo yanarejea kwa wananchi. Ni katika eneo hili la namna tulivyoanza mchakato wa kufikia lengo la kuwafikisha katika vyombo vya kisheria wahusika, ndipo leo imenilazimu kuuweka kizimbani muelekeo wa Rais na 'kamati' aliyoiunda inayoongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwanza kabisa tuliambiwa, kama ambavyo kijitabia hiki kilivyoanza kushamiri, kwamba Rais alikasirishwa sana na 'madudu' katika ripoti ya BoT ambayo hata sasa haijawekwa bayana. Nikimnukuu Katibu Mkuu Kiongozi, Bw. Phillemon Luhanjo, alisema hivi katika 'kidesa' chake kinachofupisha yale uchunguzi wa Ernst And Young ulichokibaini: " Baada ya kupitia taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali na Mkaguzi wa Nje, yaani, kampuni ya Ernst and Young. Mhe. Rais amesikitishwa na kukasirishwa na taarifa ya kuwepo vitendo vya ukiukwaji wa makusudi wa sheria, kanuni na taratibu za madeni ya nje vilivyofanywa katika taasisi muhimu na nyeti katika Benki Kuu." Kwa mujibu wa nukuu hiyo Rais, hakufurahishwa hata kidogo na wizi huo tena, kwa msisitizo, narejea neno 'wa makusudi' uliofanyika BoT.Lakini nukuu hiyo pia inaweka rekodi ya kuwa ya pili kwa wasaidizi waandamizi wa Rais kuuarifu umma hasira za kiongozi wetu. Nitaomba samahani kwa wasomaji wangu, kwamba leo katika kukasirishwa kwangu na kukasirika huko kwa Rais, nitakuwa mwanataaluma sana wakati fulani, lengo likiwa moja tu; kuhakikisha tunaeleweana vyema. Kwa ujumla nimestushwa na kasirika ya Rais jinsi inavyotafsiriwa kivitendo. Katika hilo la kamati ambayo ndiyo inatafsiri kivitendo kasirika ya Rais, kuna masuala mawili yanaonesha huenda tukaishia kwenye usanii na bilioni 133 zilizofujwa zikapotea kabisa au tukajikuta mwisho wa siku tumetumia bilioni 140 katika mchakato wa kutaka kuziokoa bilioni 133! Nasema hivi kwa nini? Mosi, muda ambao 'tume' hiyo imepewa; miezi sita unatia shaka! Pili mbinu zilizoanza kutumiwa na 'tume' hiyo; kuanza kukusanya maelezo ya wenye taarifa zozote kuhusu BoT nazo ni ngeni kabisa katika taaluma ya sayansi ya makosa ya jinai. Kwa nini natofautina sasa na Rais na watu hawa wa 'tume' hiyo. Hoja yangu ya kwanza ni kwamba kwanza ni hatari sana kumpa muda adui yako. Hili Rais Kikwete analifahamu kwa kuwa amesoma sayansi za kijeshi, mimi nilizigusa tu katika pitapita zangu za 'kukimbia umande.' Zaidi si tu kivita, bali katika hali halisi, kisheria ni jambo la hatari sana kama utampa mtuhumiwa nafasi ya kujua unakuja na kesi gani, una ushahidi gani, unautoa wapi na lini ndio utashtaki.Ndio maana kuna mamia ya watuhumiwa wanakataliwa dhamana kwa sababu tu akiwa mtaani anaweza kupata mwanya wa kuharibu ushahidi muhimu. Katika hili napata wasiwasi sana kama kuna nia ya dhati ya kufika kila Mtanzania anakotaka tufike katika hili, naanza kuhisi sanaa na usanii vitatawala katika suala hili. Mwanasheria Mkuu, Johnson Mwanyika, Inspekta Jenerali wa Polisi, Said Mwema na Mkurugenzi wa TAKUKURU, Dkt. Edward Hosea ni miongoni mwa wajumbe wa 'kamati' hiyo ambao pia wote kwa bahati nzuri ni wanataaluma wazuri wa sheria. Hao kwa taaluma zao, kama watauweka kando usanii, wanafahamu fika kuwa kesi ya BoT ni ya kihistoria katika taifa hili na ni kesi inayowahusisha watu wenye utaalamu katika maeneo walikotuhumiwa kuchota fedha na zaidi ni kesi ambayo hata hao watuhumiwa watataka waonekane wasafi mbele ya jamii; hawatakubali kufa kibudu. Ni kwa jinsi hii, nilidhani, na kwa hakika sheria zinaruhusu, kama inavyotokea kwa kesi nyingine za jinai, baada ya Rais kupatiwa ripoti kamili, wataalamu wake wa sheria wangeipitia na kuona kama kuna kesi ya msingi, kitaalamu wanaita prima fascie case. Kwa hakika kwa mujibu wa Luhanjo kama tulivyomnukuu hapo juu, katika suala la BoT kuna prima fascie case na ndio maana maneno kama 'kwa makusudi walikiuka sheria, kanuni na taratibu,' yametumika kwenye nukuu tuliyoiona hapo awali. Kwa mujibu wa utaalamu wangu mdogo wa sayansi za makosa ya jinai, kosa la jinai linapande kuu mbili ili likamilike; ile ya nia ovu (malice aforethought au malice prepence) na kitendo kamili cha kufanya jinai husika (actus reus). Bila kuingia ndani katika ripoti ya ukaguzi wa BoT, kwa ile karatasi tu yenye kurasa nane aliyoisambaza Bw. Luhanjo kwa wanahabari, ni dhahhiri kuwa makosa kamili ya jinai yametendeka BoT; kwanza ripoti imebaini 'kwa makusudi kanuni na sheria zilivunjwa.' Neno hili linaashiria kuwepo nia ovu. Na kwa kuwa ripoti imebaini kuwa sh. bilioni 133 zilifunjwa na imeyataja makampuni kadhaa yawe feki au ambayo yapo kihalalim lakini yalitumia 'njia za panya,' kupata fedha hizo tayari actus reus imetimia. Kosa kamili hapo la jinai limekamilika kutendeka. Kinachofuata kwa elimu yangu ya kabwela ni Je, kama kuna kosa la jinai limetendeka, ni lipi au ni yapi kwa kadiri ya ushahidi ambao Ernst And Young wameuambatanisha katika ripoti yao? Na swali lingine la msingi ni Je, akina nani wanahusika? Kulijibu hili nalo tunarudi pale pale kwenye nukuu ya Bw. Luhanjo, alipokiri kulikuwa na 'uvunjaji wa makusudi wa sheria.' Kama Ernst And Young walibaini uvunjaji wa makusudi, basi wanawajua au wamewataja wavunjaji hao wa makusudi. Na hata kama hawajatajwa, kitu ambacho siamini, basi kwa kupitia rejea ya nyaraka zilizoko, waliohusika kuzisaini au kuziidhinisha na watendaji wengine wote wanaohusika na mchakato wa uendeshaji wa akaunti ya EPA ni watu wa kwanza kisha wanafuatia wakurugenzi wote za zile kampuni zilizotajwa. Maswali hayo hapo juu ukimpa mtu aliyehitimu vyema darasa la Criminal Law la Profesa Ibrahim Juma, Criminal Procedure la Profesa Sifuni Mchome na Profesa Abdallah Saffari au darasa la Legal and Statutory Interpretation la Professor Issa Shivji, Administrative Law la Prof. Jwan Mwaikyusa au darasa adhimu la sheria za madhara (Torts) la Dkt. Asha-Rose Migiro, Dkt. Michael Wambari na Profesa Pallamagamba John Kabudi, kwa uchache tu, haiwezi kumchukua zaidi ya wiki kukakabidhi aina ya mashitaka yanayofaa kufunguliwa. Lakini pamoja na ushahidi mzito wa nyaraka ambao ni lazima umeambatanishwa kwenye ripoti (rejea dokezo kuwa baadhi ya risiti zilizowasilishwa na makampuni hayo BoT zilikuwa feki, kuonesha kuwa ripoti inaviambatanishi kama hivyo au vinaweza kupatikana, kama havijaambatanishwa). Na kama kuna viambatanishi vya nyaraka katika ripoti ya Ernst and Young basi tunataka ushahidi gani mzuri zaidi ya huo? Au tusema Tanzania imejivua kufuata sheria za kiingereza? Maana kama tunafuata mfumo wa sheria za kiingereza, kitaalamu mpaka sasa ushahidi bora zaidi duniani ni ule wa nyaraka yenyewe (Rejea shauri mashuhuri la Kiingereza la Omychund v Barker (1745) 1 Atk, 21, 49; 26 ER 15, 33, tazama falsafa ya Lord Harwicke katika hukumu hiyo). Inashangaza kuona kampuni yenye wataalamu imefanyakazi kitaalamu, halafu leo tunaanza kukwepa hoja na eti tunaalika wananchi wenye taarifa wazitoe. Zipi zaidi ya hizi za Ernst And Young? Ushauri wangu wa kitaalamu katika hili ni kwamba hakuna hoja wala haja ya kuuma maneno na kuwaachia wananchi zigo la 'mnyamwezi walibebe,'Hiyo ilikuwa kazi ya Ernst And Young ambayo kwa hakika wameitimiza vyema. Ni mwananchi gani ana uwezo, urahisi na fursa ya kujua taarifa za jikoni kama Benki Kuu zaidi ya vyombo vya Serikali yenyewe; wanausalama wa taifa, mafisadi wenyewe popote waliko na wafanyakazi wazalendo wa ndani ya BoT ambao tunajua walijitolea sana wakati wa uchunguzi wa kampuni ya Ernst and Young kueleza walichokijua? Huu 'uchunguzi' mwingine unaofanywa kwa kualika wananchi ambao tayari wana misongo mingine ya kimaisha, eti watoe taarifa, wakati kuna wataalamu tuliowaalika na kuwalipa mamilioni watufanyie kazi na wengine wapo nchini wanaendeleea kulipwa kila mwezi. Hii ni kuzidi kuibua maswali magumu juu ya kiwango cha kukasirika kwa Rais. Wakati watanzania wakitafakari kukasirika huko kwa Rais na watu kama sisi tukiamua kukasirikia kukasirika huko kwa Rais, wengi hawajasahau rejea ya msingi ambayo inapaswa kutosahaulika katika nchi hii na sisi tunaokumbuka ya nyuma katika kuangalia yaliyopo na kuakisi yajayo, hatujaisahau. Rais Kikwete alipopokea ripoti ya uchunguzi juu ya mauaji ya wafanyabiashara wa Mahenge, Morogoro (waliotuhumiwa kuwa majambazi), ndani ya saa 48 tu mtuhumiwa mkuu, Bw. Abdallah Zombe alikamatwa na wenzake (wakati uchunguzi ukiendelea). Mafisadi wa BoT nao, ili, kama nilivyogusia, wasipate nafasi ya kufanya ufisadi zaidi, hawakupaswa kupewa muda, wangechukuliwa hatua za haraka kama ilivyokuwa kwa akina Zombe, wakati uchunguzi unaendelea, hilo sheria inaruhusu. Lakini sasa miezi sita hii inaibua maswali magumu na kwa hakika watawala wetu wanalazimika kupanda kizimbani, kizimba cha hoja kujibu: Miezi sita yote hii ya nini? Kwa maoni, ushauri: simu 0713 584467

FEEDBACKS/RECOMMENDATIONS/SUGGESTIONS WRITE HERE

How did you hear about us?
Please give us your recommendations about our services in the space provided below.
Name:
Email Address:

create form

Mashauri Musimu

Mashauri Musimu
SOLICITOR-Ilala Municipal Council